Bismilah Rahman Raheem
Assalaam alaykum warahmatullahi wa barakaatuhu.
Taarifa hii inahusu tukio lilitokea jana Mina Saudi Arabia
wakati mahujaji wakielekea kwenye Jamaraat , palitokea msongamano mkubwa (
stampede) na kupelekea mahujaji zaidi ya 700 kufariki na mamia kadhaa
kujeruhiwa.
Tayari tumethibitisha kutokea vifo vya watu watano waliotokea
Tanzania miongoni mwao mmoja ni raia wa Kenya na wengine wanne ni
Watanzania.
Watanzania waliotambuliwa hadi jana usiku wametajwa kuwa ni Bi
Mwanaisha Hassan Juma, Mkungwe Suleiman Hemedi na Sefu Saidi Kitimla.
Mwanamke mwingine mmoja Mtanzania jina halijaweza kupatikana
hadi Alhamisi usiku wakati tukiandaa taarifa hii.
Raia wa Kenya ametambuliwa kwa jina la Bi Fatuma Mohammed Jama.
Kuna taarifa ya mahujaji wanawake wawili ambao hadi Alhamisi
usiku walikua hawajapatikana hivyo hatukua na uhakika juu ya usalama wao hadi
tutakapowaona ama kupata taarifa zao. Ifahamike kuwa majina yamepatikana kupitia vitambulisho vyao
ambavyo wahanga wa tukio hili waliweza kuvichukua kutoka kwenye miili ya
marehemu.
Nimepokea taarifa za majeruhi miongoni mwa mahujaji wetu wa Tanzania na baadhi ya majeruhi hao nimeonana nao mara baada ya kuruhusiwa kutoka hospitalini.
Vilevile nimeagiza maafisa wetu wa Bakwata nilionao hapa Mina
kuendelea kufuatilia habari na taarifa za mahujaji wetu katika hospitali na sehemu
za kuhifadhia maiti. Nimefanya hivyo ili niweze kuwa na uhakika juu ya usalama wa
mahujaji wetu.
Katika kipindi hiki cha taharuki kubwa tunafanya mawasiliano na
wizara husika hapa Saudi Arabia kwa kushirikiana na serikali yetu kupitia
ubalozi wetu hapa Saudi Arabia. Natambua uwepo wa mkanganyiko wa taarifa ambazo zinazidisha
taharuki kwa ndugu na jamaa wa mahujaji wetu. Nachukua fursa hii kuwaomba ndugu na jamaa wa mahujaji kuwa
watulivu na kuwa na subra katika wakati huu mgumu sana kwetu sote.
Tunaendelea kufuatilia kwa karibu sana na Insha Allah mara tu
tukipata taarifa za uhakika basi tutawafahamisha.
Kutokana na idadi ya maiti kuwa kubwa serikali ya Saudi Arabia
wanaendelea na zoezi la kutambua uraia wa kila mwili ili waweze kutoa taarifa
tunatarajia wakati wowote tutakuwa tumepata taarifa zaidi.
Wabillahi Tawfiiq.
Sheikh Abu Bakari Zuberi
Mufti wa Tanzania.
MECCA, Saudi Arabia
Baadhi ya Watanzania walioko Hijja na ambao wamenusurika na maafa ya msongamano wa watu huko Mina jana. Kulia nia Bw. Yahaya Sameja, kushoto ni mwigizaji mchekeshaji Bw. Amri Athumani al maarufu kama King Majuto. Wa katikati jina lake halikuweza kupatikana.
No comments:
Post a Comment