Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Friday, October 23, 2015

MAALIM SEIF AUNGURUMA KATIKA VIWANJA VYA MAISARA NA KUFUNGA KAMPENI

         Na: Hassan Hamad, OMKR. 

Chama Cha Wananchi CUF kimefunga rasmi kampeni zake za uchaguzi kwa upande wa Zanzibar na kuwataka wadau wa uchaguzi kuheshimu maamuzi ya wananchi katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Jumapili ijayo.
Akizungumza kwenye mkutano huo wa ufungaji wa kampeni uliofanyika viwanja vya Maisara Mjini Zanzibar, Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia Chama hicho Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, amesema wananchi ndio wenye mamlaka ya kuiweka Serikali madarakani, hivyo maamuzi watakayoyafanya kwenye uchaguzi huo hayana budi kuheshimiwa.
Amerejea kauli yake ya kukubali matokeo iwapo uchaguzi utafanyika kwa uwazi, huru na haki na kuwashauri wagombea wengine wa Urais kutoa kauli kama hiyo ili kuwaondoshea hofu wananchi.


Hata hivyo amesema hatoridhia matokeo iwapo atashinda uchaguzi huo, na kuelezea matumaini yake ya kupata ushindi mkubwa katika uchaguzi ujao.

Aidha amesema atatumia uwezo wake kuviimarisha vikosi vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na hana nia ya kumfukuza kiongozi yoyote wa vikosi hivyo.



Amemshauri Rais Kikwete na Dkt. Shein kuweka mazingira mazuri ya uchaguzi ili kuhakikisha kuwa uchaguzi ujao unafanyika katika hali ya Amani na usalama.
Amesema uchaguzi usiwe sababu ya kuvurugika kwa amani iliyopo na kuwataka wananchi kushiriki kikamilifu kuhakikisha kuwa amani iliyopo inalindwa.
Amewataka wananchi kuondosha hofu wanapokwenda kupiga kura na kumchagua kiongozi wanayemtaka, na kwamba hakuna mwananchi atakayefuatiliwa au kujulikana taarifa zake.
Nae Mgombea Mwenza wa Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chadema Mhe. Juma Duni Haji amesema ana imani kuwa Watanzania wako tayari kwa mabadiliko.
Amesema iwapo wananchi watawachagua wagombea wanaotokana na Umoja wa Ukawa wataendeleza maridhiano na umoja wa wananchi, sambamba na kurejesha katiba iliyopendekezwa na wananchi ambayo itato haki kwa wananchi wote.
 Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Timu ya Kampeni ya CUF Mansour Yussuf Himid, amewataka wananchi kumchagua Maalim Seif ili aweze kuleta mabadiliko ya kiuchumi nchini.
Amesema Maalim Seif ni kiongozi anayejiamini, jasiri na mwenye uwezo wa kuongoza nchi, na kwamba iwapo wazanzibari watafanya maamuzi sahihi watajionea mabadiliko kwa kipindi kifupi baada ya uchaguzi.

No comments:

Post a Comment