Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Tuesday, January 26, 2016

Kampuni ya Reli Tanzania kuhamishia huduma zake za usafirishaji mjini Dodoma


Uongozi wa Kampuni ya Reli Tanzania (TRL)  umetangaza kuhamishia mjini Dodoma huduma zake za usafirishaji  kuanzia Ijumaa ya wiki hii Januari 29, 2016.
Taarifa hiyo imebainisha  kuwa huduma hizo zinahamishiwa kwa muda mjini Dodoma hadi pale kazi ya ukarabati ya tuta la reli litakapo tengemaa kati ya Stesheni za Kidete na Kilosa mkoani Morogoro.
Halikadhalika kutokana na mafuriko ya eneo hilo kutojulikana lini yataisha, Uongozi umeamua kwa sasa kusitisha zoezi la ukarabati ili kuokoa rasilimali zinazotumika katika ukarabati wa eneo hilo. Hata hivyo kazi ya kuzuia uharibifu zaidi dhidi ya tuta la reli inaendelea kulingana na hali inavyojitokeza. 
 Wakati huo huo Uongozi wa TRL umeandaa utaratibu na Wamiliki wa mabasi kuwasafirisha abiria wake watakaotumia huduma zake zinazoanzia siku za Jumanne na Ijumaa mjini Dodoma kutokea Dar es Salaam.


Sehemu ya uta la reli  kati ya Stesheni za Kidete na Kilosa mkoani Morogoro ambalo limesombwa na mafuriko ya maji.

 
Mafundi wakielekea sehemu ya tatizo kwa kutumia viberenge
Taarifa imefafanua kuwa wakati maombi ya huduma za kusafirisha shehena yataanza kupokelewa Ijumaa Januari 29, 2016 hata hivyo  treni ya kwanza ya abiria imepangwa kuondoka saa 2 usiku siku ya  Jumanne Februari 2, 2016 Dodoma..
Kwa taarifa hii TRL inawatangazia wananchi kwa ujumla kuwa wanaweza kuanza kukata tiketi za safari ya Jumanne wakati wowote mara baada kusoma taarifa hii katika stesheni za reli ya kati   zilizo karibu  yao.

Uzoefu unaonesha katika miaka ya 1998 na 2010 huduma za reli zilihamishiwa Dodoma kwa muda baada ya eneo kati ya Gulwe, Godegode mkoani  Dodoma , Kidete na Kilosa mkoani Morogoro  kukumbwa na mafuriko makubwa na kuisambaratisha njia ya reli kabisa katika maeneo hayo. 
Taarifa imefafanua kuwa japo hatua hiyo itaongeza gharama lakini ni muhimu kwa huduma za usafirishaji ziendelee ili kusaidia Watanzania  kichumi na kijamii kadri inavyowezekana. Imefahamika kuwepo  huduma ya  reli kunapunguza kasi ya uharibifu wa barabara zetu ambazo sio muda mrefu zimejengwa kwa gharama kubwa kutokana na fedha za walipa kodi wa Tanzania.

Imetolewa na Afisi ya Uhusiano kwa niaba ya
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TRL Mhandisi Elias Mshana.
Dar es Salaam,Chanzo Issa Michuzi

No comments:

Post a Comment