Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Friday, March 27, 2015

Mazoezi Stars yavuta mashabiki Mwanza

PICHA NA MAKTABA


Mashuti makali yaliyopigwa na wachezaji wa timu ya Taifa Stars kwenye mazoezi yao kwenye Uwanja wa CCM Kirumba yamewavutia mashabiki wachache waliofika ili kufuatilia mazoezi hayo.

Baadhi yao wametamka kuwa kama wakiyatumia Jumapili kwenye pambano na Malawi, basi wataondoka na kapu la mabao.

Stars wanafanya mazoezi jijini hapa tangu juzi na kwa muda mwingi juzi walipiga mashuti ambayo 
 
makipa Aishi Manula na Mwadini Ally, wote kutoka Azam waliokaa magoli tofauti walikuwa na wakati mgumu.

Washambuliaji wa Stars, Mbwana Samatta,Thomas Ulimwengu, John Bocco walikuwa mwiba mkali kwa makipa hao kutokana na mashuti makali waliyopiga, kufunga huku mengine wakiyapangua.

Katika mazoezi hayo, Samatta aliwakosha mashabiki baada ya kuruka kichwa maridadi na kumfunga kipa Mwadini Ally ambaye hakufanya chochote zaidi ya kuuangalia mpira ukiingia wavuni.

Kocha John Tegete wa Toto African ya hapa aliyekuwa uwanjani hapo alisema kuwa kocha wa Stars, Martin Nooij katika mazoezi hayo amekuwa akiwaelekeza mbinu za kila mchezaji kufunga.

“Hii safi, naona muda mwingi kocha anafundisha namna ya kila mmoja kufunga bao, si beki wala mshambuliaji, wote wanafunga, ndiyo maana unaona muda mwingi ameutumia kufanya hili zoezi inapendeza,” alisema Tegete.

Wadau wa soka jijini hapa, Juma Kosky, Kadiri Ramadhani na Issa Ally walisema kuwa mazoezi hayo yamewapa faraja kuwa mechi hiyo haitatakuwa ngumu kutokana na morali ya wachezaji hao, hasa Samatta.

“Kama haya mashuti wanayopiga wakiyafanya kwenye mechi yetu ya Jumapili na hao Malawi, basi kazi itakuwa rahisi, wamenikosha, ila wachezaji wanatakiwa kuyafanya yale ambayo wameelekezwa mazoezini, tumeona morali yao iko juu,” walisema mashabiki hao.

No comments:

Post a Comment